Habari zilizopatikana na kuthibitishwa na Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, Prodenciana Protas zinaeleza kuwa ajali hiyo ilitokea saa 2.00 usiku wa kuamkia jana wakati coaster hiyo ikitokea Iringa kwenda Njombe dereva wake kugongana na lori wakati akijaribu kuyapita magari zaidi ya matatu eneo la mlimani.
Hii ni ajali ya pili kutokea katika barabara hiyo baada ya basi la Majinja kupata ajali na kuua zaidi ya watu 50 wakati likitokea Mbeya kwenda Dar es Salaam miezi mitatu iliyopita.
Kaimu Kamanda, Protas alisema lori hilo mali ya Kampuni ya Bravo Logistic T (Ltd) ya Dar es Salaam lilikuwa likiendeshwa na Rogers Mdue (33) mkazi wa Mwanza na Nico Mangula (29-30) makazi wa Makambako.
Alisema kati ya watu 23 waliokufa katika ajali hiyo 16 ni wanaume, watoto watatu na wanawake saba huku majeruhi wakiwa 34, kati yao wanaume 18, wanawake 16 na watoto wawili na maiti 12 zimetambuliwa na ndugu.
Aliwataja majeruhi 30 ambao majina yao yametambuliwa kuwa ni Emma Lupembe (53) mkazi wa Iringa, Veronica Simba (20) mkazi wa Tabora aliyekuwa akielekea katika mafunzo ya JKT-Mafinga na Shadia Allu (24) mkazi wa Iringa.
Pia, wamo Mariamu Mbise (23) mkazi wa Mafinga Kinyanambo B, Anita Makwela (24) mkazi wa Dabaga Kijiweni, Benita Sagara (18) mkazi wa Njombe, Bertha Mkoi (27) mkazi wa Mafinga akiwa na mwanaye wa miaka minne aliyefariki, Rahel Mavika (18) mkazi wa Ihanzutwa Mufindi, Selina Flugensi (23) mkazi wa Kibondo mkoani Kigoma aliyekuwa akienda JKT katika Mafunzo na Maria Mwenda (17) mkazi wa Mafinga.
Wengine ni Ndipako Mbilinyi (28) mkazi wa Njombe, Alexander(28) mkazi wa Mafinga, Simon Jumbe (22) mkazi wa Singida, Meshacky Kibiki (44) mkazi wa Mafinga, Jerry Lutego (36) mkazi wa Mafinga, Enock Kanyika (18) mkazi wa Mafinga na Yusuph Lulandala (22) mkazi wa Njombe.
Pia, wamo Deogratias Kayombo (21) mkazi wa Kiloleni Tabora aliyekuwa akielekea katika mafunzo JKT Mafinga, Petro Mwalongo (21) mkazi wa Njombe, Paul Chahe (21) mkazi wa Idete Kilolo Iringa aliyekuwa akienda JKT Mafinga katika Mafunzo na Kenedy Msemwa (28) mkazi wa Njombe.
Kaimu Kamanda aliwataja wengine ni Emmanuel Anthon (21) mkazi wa Mwanza, Mode Shilazi mkazi wa Singida, Godfrey Kanyika (39) mkazi wa Mafinga, Boniface Bosha (20) mkazi wa Sumbawanga Ambiana Meshack (35) mkazi wa Njombe ambaye ni mkaguzi wa basi hilo la Another G.
Matha Kanyika (30) mkazi wa Mafinga akiwa na mwanaye wa miezi miwili na nusu, Melika Tonga miezi miwili na nusu ambaye ni mtoto wa Martha Kanyika, Yusuph Luhumba (34) Mwanasheria mkazi wa Mafinga, Damian Kuyala (42) mkazi wa Itamba Iringa, pia wanaume wawili na wanawake wawili ambao hawajatambuliwa kutokana na hali zao kuwa mbaya.
Kaimu Kamanda huyo alitaja majina ya maiti zilizotambuliwa kuwa ni Lucas Pangras, Blasto Salima, Dickison Luvanda, Albert Silla ambaye ni askari wa Ruvu JKT na dereva wa lori lililogongana na basi hilo, Rogers Mdoe.
Wengine ni Eva Mbalinga, Khadija Mkoi mtoto mdogo wa miaka minne, Clemence Mtati, Mohamed Kalika, Castory Mwakiamba (30) mkazi wa Iringa, Damiana Myala na Silo Nziku (29) mkandarasi wa Ipogolo Iringa
Majeruhi
Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi majeruhi wa ajali hiyo, John Lutego na Emma Lupembe walisema kabla ya kutokea dereva wa basi hilo la Another G alikuwa ametoka kujaza mafuta katika kituo kilichopo eneo la Kinyanambo A na baada ya hapo alianza kushuka mteremko kwa kasi ili kupanda mlima kirahisi.
Lutego alisema wakati dereva wa basi hilo akiwa ameliachia basi lake mbele kulikuwa na magari matatu pamoja na bajaji yakipanda mlima kwa mwendo wa kawaida.
Alisema alifanikiwa kuyapita na wakati akitaka kuipita Bajaji iliyokuwa mbele wakati akijiandaa kumaliza mlima huo ghafla alikutaka na lori ambalo lilikuwa likianza kushuka mlima kwa kasi.
“Kilichotokea baada ya dereva wa lori kuona dereva wa basi hilo la Another G likiwa limehama upande wake na kupita upande wa pili wa barabara alilazimika kujaribu kumkwepa ila ilishindikana baada ya dereva huyo wa basi kuonesha msimamo wa kubaki eneo ambalo si lake kabla ya kugongana uso kwa uso,” alisema.
Lupembe alisema chanzo cha ajali hiyo mbali ya uzembe wa dereva wa basi hilo kutaka kuyapita magari mlimani ambako kuna alama zinazozuia kupita gari lililopo mbele bado dereva huyo wa basi la abiria alikuwa katika mwendo mkali zaidi.
Hata hivyo, alisema basi hilo lenye uwezo wa kupakia abiria 41 pekee lilikuwa limezidisha abiria.
Mkuu wa Wilaya
Mkuu wa Wilaya ya Mufindi, Mboni Mhita akizungumzia ajali hiyo baada ya kuwatembelea majeruhi alisema ni ajali mbaya kutokea katika wilaya yake kwa kipindi kifupi cha miezi kama mitatu tangu Watanzania zaidi ya 50 wapoteze maisha yao kwa ajali kama hiyo.
Alisema baada ya kupata taarifa ya ajali hiyo alifika eneo la tukio akiwa na kamati yake ya ulinzi na usalama kwa ajili ya kuokoa majeruhi na kuweka ulinzi wa mali za majeruhi hao na wale waliopoteza maisha.
Mhita alisema chanzo cha ajali hiyo ni uzembe wa dereva wa basi la abiria ambaye alikuwa akitaka kuyapita magari zaidi ya mawili na bajaji katika mlima na kwamba dereva wa basi hilo baada ya kutokea ajali alikimbia na baadaye alikamatwa na Jeshi la Polisi huku dereva wa lori akifariki dunia.
“Ilichukua muda mfupi zaidi mimi kama Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama na Mkuu wa Wilaya hii ya Mufindi kufika eneo la tukio cha kwanza ilikuwa ni kuokoa maisha ya majeruhi wote na baada ya hapo kusafirisha maiti zote na kuona mali zao zipo salama, kwani katika matukio kama haya vibaka hujichanganya ili kupora mali mbalimbali,” alisema.
Mganga mkuu
Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya ya Mufindi, Dk. Godluck Mlimbila alithibitisha kupokea maiti 22 usiku wa kuamkia jana huku majeruhi mmoja ambaye ni mtoto mdogo akiongezeka kufariki usiku akiwa katika matibabu hospitalini hapo.
Kuhusu majeruhi waliopokelewa, alisema majeruhi 34 ndiyo walipokelewa na majeruhi saba kati yao waliruhusiwa baada ya hali zao kuendelea vizuri na kati ya majeruhi 34, majeruhi 27 ndiyo ambao wanaendelea kupatiwa matibabu na majeruhi wanne kati ya hao 27 hali zao ni mbaya na wanatarajiwa kuhamishiwa Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Iringa.
